CHAMA CHA CUF UPANDE WA KATIBU MKUU MAALIM SEIF WATOA REPORT NA UFAFANUZI JUU YA MIGOGORO INAYOIKABILI CHAMA HICHO.

Wakiongea na waandishi wa habari viongozi wa CUF upande unaomuunga katibu mkuu wa chama cha hicho Mh Maalim Seif umefafanua kwa kina mambo mbalimbali kuhusu migogoro inayoikabili na msimamo wao kutokana na matatizo hayo. 

Mh:Mbarala Maharagande Naibu Mkurugenzi wa Habari wa Chama cha Wananchi (CUF),, alizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam na kutoa taarifa hiyo.

CUF WEEKLY REPORT – RELEASED ON DATED 8TH-13TH, AUGUST, 2017 


1. MAHAKAMA KUU IMESAJILI MAOMBI YA WABUNGE CUF. 

2. MHE. BASHANGE AWAFUNDISHA KATIBA YA CUF JAJI MTUNGI, NA SPIKA NDUGAI. 

3. LIPUMBA AIFANYIA KAMPENI CCM ISHINDE NAIBU MEYA MANISPAA YA MTWARA

4. MDAHALO MPANA WA KATIBA YA CUF WAANDALIWA.

 

THE CIVIC UNITED FRONT

(CUF–Chama Cha Wananchi)


THE DIRECTORATE OF INFORMATION, PUBLICITY AND PUBLIC RELATION

P.O.BOX 10979 DAR ES SALAAM  


TAARIFA KWA UMMA NA VYOMBO VYA HABARI


MAPITIO YA TAARIFA MUHIMU ZA WIKI TAREHE 08TH -13th AUGUST, 2017


KURUGENZI ya habari wiki hii inapenda kuwajulisha masuala na matukio yafuatayo yaliyojitokeza na au kupangwa kufanyika kama ifuatavyo:   


1. KUHUSU TAARIFA YA KESI/MASHAURI YANAYOENDELEA MAHAKAMANI:

a) Jana Jumatatu tarehe 7/8/2017 Msomi wakili Peter Kibatara alikamilisha taratibu za kusajili shauri dogo la madai [Miscelleneous Civil Application] na kupewa namba ya usajili 479 na kurejeshwa kusikilizwa kwa Mheshimiwa Jaji Lugano Mwandambo ambaye ndiye atasikiliza shauri la msingi namba 143/2017 lililopangwa kusikilizwa/kutajwa Tarehe 31/08/2017, katika shauri hilo Wabunge 8 na madiwani wawili wanaiomba mahakama itoe Amri ya zuio la muda [Order of Temporary Injuction and To maintain Status Quo] ili hali iendelee kubaki kama ilivyo sasa mpaka pale shauri la msingi litakaposikilizwa na kuamuriwa. Taratibu za kimahakama zikikamilika tutawajulisha imepangwa kusikilizwa lini. 

b) Tarehe 11/8/2017 siku ya Ijumaa mbele ya Mheshimiwa Jaji Wilfred Ndyansobera kutakuwepo na mashauri 5 yatayopangiwa utaratibu wa kusikiliza na au kutajwa pamoja na kutolewa Maamuzi ya pingamizi lililowekwa na Lipumba na wenzake katika shauri dogo namba 28/2017 kuhusu Amri ya Zuio la kutolewa fedha za Ruzuku ya CUF. Mashauri hayo ni;

• Shauri la msingi la madai (Civil Application No. 21/2017)

kuhusu wizi wa Ruzuku ya CUF shilingi milioni 369.

• Shauri la Madai Namba 13/2017 Lililofunguliwa Na Ally Salehe

dhidi ya RITA, Lipumba na wenzake kuhusu uhalali wa Bodi FEKI ya

Wadhamini ya CUF iliyosajiliwa na RITA. 

• Shauri dogo Namba 51/2017

linaloomba kuwepo kwa zuio (Injuction) dhidi ya bodi hiyo kufanya

kazi mpaka shauri la msingi litakaposikilizwa na kufanyiwa maamuzi.

• Shauri la Jinai namba 50/2017 kuhusu Lipumba na wenzake, Emmy

Hudson -RITA, Jaji FRANCIS Mutungi kughushi nyaraka na kutaka

kuingilia mwenendo wa mashauri yaliyopo Mahakama (CONTEMPT OF COURT

PROCEEDINGS)


2. MHE.JORAN BASHANGE ATOA UFAFANUZI WA HOJA NA MAJIBU/TAARIFA YA MSAJILI WA VYAMA NA SPIKA WA BUNGE KUHUSU MAMLAKA YA KATIBU MKUU WA CHAMA MAALIM SEIF SHARIF HAMAD:


Kaimu Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara aliyeteuliwa na Baraza Kuu la Uongozi wa Taifa Tarehe 28/8/2016 baada ya kumchukulia hatua za kinidhamu za kumsimamisha uanachama aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara Magdalena Sakaya ambaye baada ya maamuzi hayo alikata Rufaa kwa Mkutano Mkuu wa Taifa. Kama inavyoeleza Katiba ya CUF Ibara ya 83(7) “Endapo Baraza Kuu la Uongozi la Taifa litapomvua madaraka mjumbe wa Bodi ya Wadhamini au NAIBU KATIBU MKUU, litalazimika kumteua mjumbe mwingine wa Bodi ya Wadhamini au kumchagua Naibu Katibu Mkuu mwingine kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii katika kikao chake kinachofuata ikiwa muhusika hakukata Rufaa kwa Mkutano Mkuu wa Taifa.”


Mhe. Bashange ambaye pia ni MKURUGENZEI WA FEDHA NA UCHUMI NA KATIBU WA BODI YA WADHAMINI YA CUF; Ameeleza mbele ya waandishi wa Habari kuwa hoja zilizotolewa katika majibu ya barua ya Msajili Francis Mutungi na ofisi ya Spika wa Bunge hayana mashiko ya kisheria na Kikatiba na kwamba katiba ya CUF haina Cheo cha ‘KAIMU KATIBU MKUU’ na badala yake yeyote atakayetekeleza majukumu ya Katibu Mkuu pale asipokuwepo ofisini au hata akiwepo ofisini atatekeleza majukumu hayo KWA NIABA YA KATIBU MKUU TU. NAFASI YA KAIMU KATIBU MKUU iliyoelezwa katika Katiba Ibara 93(3) ni dhamana ya utekelezaji wa majukumu ya KATIBU MKUU na wala hayapokonyi mamlaka na madaraka ya KATIBU MKUU. Kinachoendelea sasa kwa Lipumba, Msajili na genge lao ni upotoshaji wa Tafsiri sahihi ya Katiba ya CUF ili kukidhi malengo wanayokusudia ya kukihujumu Chama. Maalim Seif ndiye KATIBU MKUU wa CUF na anatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba ya CUF akiwa katika ofisi ya CUF MAKAO MAKUU Mtendeni, Zanzibar. Na Tanzania Bara anatekeleza majukumu yake akiwa katika ofisi yake iliyopo ndani ya ofisi ya Wabunge CUF, Magomeni-Dar es Salaam. Mhe. Bashange ameeleza kuwa hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa kudhibiti hali hiyo. 


3. LIPUMBA NA MAFTAHA NACHUMA WAIFANYIA KAMPENI CCM ISHINDE NAFASI YA NAIBU MEYA KUTOKA CCM MANISPAA YA MTWARA MIKINDANI:


Wiki iliyopita Manispaa ya Mtwara Mikindani ilifanya uchaguzi wa Naibu Meya kwa mujibu wa kanuni za TAMISEMI kila mwaka Naibu Meya uchaguliwa upya. Baada ya uchaguzi Mkuu Mkuu 2015 CUF na CHADEMA walishirikiana kuunda Manispaa hiyo kwa CUF kutoa Meya [Mheshimiwa Mstahiki Godfrey Mwachise] na CHADEMA kutoa NAIBU MEYA [Mheshimiwa Mstahiki Eric Mkapa] hii ilitokana na matokeo ya ushindi wa madiwani ambapo CUF iliongoza kwa kuwa na madiwani 8 wa kata na 3 viti maalumu=11 ukijumlisha na Mbunge 1 jumla kura 12. CHADEMA walipata madiwani 3 wa kata na mmoja viti maalumu na Mbunge mmoja wa Viti maalum jumla kura 5 [diwani mmoja alifariki] wamebaki 4. CCM walipata Madiwani 7 wa kata na viti maalumu 3 jumla madiwani 10. 


MATOKEO BAADA YA LIPUMBA KUREJESHWA NA MSAJILI NDANI YA CUF NA KUUNDA UMOJA RASMI CUF+CCM=UCUFCCM:

Lipumba na Maftaha wakapanga mkakati wa kuisaidia CCM ishinde ikiwa ni kurejesha fadhila ya jinsi CCM na serikali zake zinavyowasaidia kufanikisha kutekeleza PROJECT waliyokubaliana ya kuihujumu CUF na UKAWA kwa kumuagiza Katibu wa Wilaya Mtwara Mjini awasilishe jina la Mgombea wa CUF ili kuzigawa kura. Pili, walihakikisha baadhi ya madiwani hawahudhurii katika kikao hicho na kugharamika kuwapa posho zao zote ili kuondoa kura. Maftaha akiongoza kutohudhuria kikao hicho cha uchaguzi. Wale waliohudhuria kwa lengo la kuhalalisha kolamu ya kikao walilazimishwa kuipigia kura CCM na kama hawawezi basi waipigie kura CUF ili kuzigawa kura hizo; 


MATOKEO YA UCHAGUZI WA NAIBU MEYA:

CCM KURA 15 -  NDUGU SHADIDA NDILE [ameshinda] 

CUF KURA 7   - Mgombea SULEIMAN ISSA MSHAMU

CHADEMA KURA 5- Mgombea ERIC MKAPA


Haya ndiyo anayoyapigania Lipumba na kundi lake kwa sasa baada ya ‘Struggle’ ya miaka 25 ya mapambano dhidi ya kudai HAKI, USAWA, DEMOKRASIA, UWAJIBIKAJI, KUPIGA VITA DHULMA, UKANDAMIZAJI, UBAGUZI, UONEVU uliokuwa unafanywa na CCM na serikali zake ndani ya miongo 5[miaka 50] toka tupate uhuru.  Mapambano hayo yamegharimu maisha ya watanzania, maisha ya WANACUF, Mauaji, Kufungwa, Kuwekwa Vizuizini, Vipigo, Kupata Ulemavu, Kuharibiwa Mali Na Biashara, Vitendo Vya Ubakaji, Kukimbia nchi na kuishi uhamishoni, Kufilisika na kuharibikiwa mustakbali wa maisha ya watu na familia zao na hata ndoa kuvunjika. 


Watanzania leo eti wanataka kuaminishwa na Lipumba na genge lake kuwa UKAWA haufai. CCM ndio inayofaa kushirikiana nao. Lipumba ameratibu ushindi wa Naibu Meya wa CCM  Mtwara.  Huyu ndio yule Full Bright International Visiting Professor Ibrahim Haruna Lipumba Nguyuri kutoka Ilolanguru, Mpingo wa Tabora tuliyeishi nae kiasasa na kumuamini kwa kipindi cha takribani miaka 20, amekubali kutiwa bei, amekubali kutumika, aliyesaliti mapambano ya kudai HAKI SAWA KWA WOTE.


4. MDAHALO JUU YA KATIBA YA CUF:

Kituo kimoja cha Television na Radio nchini kipo katika maandalizi ya mwisho kuandaa mdahalo mpana juu ya Katiba ya CUF na masuala yanayoendelea kutokana na upotoshaji unaofanywa na wenye nia ovu dhidi ya CUF. Hatua hiyo imekuja baada ya Mkurugenzi wa Habari- Mhe. Salim Bimani kufanya mazunguzo rasmi na uongozi wa Kituo hicho mapema wiki hii.  Tunatoa wito kwa wanaCUF, wananchi na wadau mbalimbali watakaopenda kushiriki mjadala huo kutujulisha na kutuandikia maeneo ya msingi ambayo wangependa kupata ufafanuzi wake. Hatua hii itawasaidia watanzania na wadau wa masuala ya kisiasa nchini kwa ujumla kujua kwa mapana dhana na Tafsiri sahihi za Ibara za Katiba za CUF (Concept and Interpretation of CUF’s Constitution). Ni matarjio yetu kuwa wenzetu watajiandaa na kuja na hoja na sio kurukaruka bila ya mpangilio kama ilivyojitokeza Azam TV wiki iliyopita. 


Mwisho:


Tunapenda kuwajulisha Wanachama na Viongozi wote wa CUF –kichama na kiserikali (Wabunge, Madiwani, wenyeviti wa serikali za mitaa nk) Msimamo wa Chama unaotokana na Baraza Kuu la Uongozi laTaifa ni kuwa Tutaendelea na mapambano haya ya kudai haki ndani ya Chama na nje ya Chama gharama yeyote ile, na kwa njia za kisiasa na kisheria kwa mujibu wa sheria za nchi na Katiba ya CUF. Hakuna mazungumzo na Wasaliti na Vibaraka kwa namna yeyote ile. Vyombo vyote vya Dola vilivyo nyuma ya Wasaliti kamwe haviwezi kuturudisha nyuma na kutukatisha tamaa. Tunapita katika kipindi kigumu cha mapambano ambayo yanatupitisha katika chujio la kuwajua wakweli na wababishaji. Tutapinga dhulma na ukandamizaji unaofanya na Serikali za CCM mpaka tutakapoingizwa katika makaburi yetu.  Utulivu, Subira Na Uvumilivu, Umoja Na Ushirikiano, Umakini na Ufuatiliaji kwa Vitendo kwa yale Majukumu Tunayojipangia na Kumtegemea Muumba wa Mbingu na Ardhi Pekee,  ndizo SILAHA zitakazotupa ushindi wa mapambano haya. UKOMBOZI wakati wote wa historia ya mwanadamu haujawahi kusimamiwa na watu wa hovyohovyo, wenye fikra na maono duni na wenye kutanguliza mbele maslahi yao binafsi dhidi ya maslahi mapana ya umma kwa kizazi cha sasa na kijacho. 


CUF NI TAASISI IMARA, YENYE VIONGOZI MAKINI. INAWATAKIA NDUGU NA MAJIRANI ZETU WA KENYA UCHAGUZI MWEMA UNAOFANYIKA LEO NCHINI MWAO. TUNARAJI UCHAGUZI HUO UTAKUWA HURU, UWAZI NA HAKI.


HAKI SAWA KWA WOTE


Imetolewa na Kurugenzi ya Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma-CUF Taifa


SALIM BIMANI

MKURUGENZI- 0777414112 / 0655 314 112


MBARALA MAHARAGANDE

NAIBU MKURUGENZI- 0715 062577 / 0767 062 577

maharagande @gmail.com

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment

0 comments:

Inaendeshwa na Blogger.

Wanaofuata

TANGAZO

My Blog List